Angola na Tanzania Zajadiliana Ushirikiano Sekta ya Mafuta na Gesi Asilia
Dar es salaam.
Balozi wa Angola nchini Tanzania, Mhe. Sandro Renato Agostinho De Oliveira
amefanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli
Tanzania (TPDC), Dkt. James Mataragio kuangazia maeneo mbalimbali ambayo
Angola na Tanzania wanaweza kushirikiana hususan katika Sekta ya mafuta na gesi
asilia.
Akizungumza katika kikao hicho, Balozi Sandro alieleza nia ya Serikali ya Angola
kuanzisha ushirikiano na Serikali ya Tanzania katika sekta ya mafuta na gesi ambayo
Angola ina uzoefu wa miaka mingi, “Angola tuna uzoefu wa miaka mingi katika sekta hii
ya mafuta na gesi na tunaamini kwa kushirkiana na Tanzania tunaweza kubadilishana
uzoefu na ujuzi katika tasnia hii” alieleza Balozi Sandro.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Dkt. James Mataragio alieleza hatua
mbalimbali ambazo Tanzania imepiga katika tasnia hii ikiwemo ujenzi wa miundombinu
ya kuchakata na kusafirisha gesi asilia pamoja na kuwa na matumizi ya gesi asilia
ambapo hadi sasa asilimia 62% ya umeme nchini unazalishwa na gesi asilia.
‘’Tunatambua kuwa Angola wamepiga hatua kubwa katika Sekta hii na tumezungumza
na Mheshimiwa Balozi kuona Kampuni zetu za Mafuta yaani TPDC kwa upande wa
Tanzania na Sonangol kwa upande wa Angola zinakuwa na ushirikiano wa karibu ili
kubadilisha uzoefu na ujuzi katika tasnia hii,’’ alieleza zaidi Dkt. Mataragio.
- By:admin
- 0 comment