Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. James Mataragio amekagua kazi za ujenzi wa kituo cha kujazia gesi asilia kinachojengwa katika barabara ya Sam Nujoma mkoani Dar es Salaam na kumtaka Mkandarasi kuongeza kasi ya utekelezaji wa mradi kwa kuongeza rasilimali watu na vifaa.

Dkt. Mataragio amesema hayo tarehe 01.01.2024 alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa mradi huo. Amesema watanzania wanasubiri mradi husika kwa hamu kubwa hasa katika kipindi hiki ambacho agenda kuu ya Serikali ni matumizi ya nishati safi na salama.

Amesema kituo hicho ndiyo kitakuwa kituo mama cha kujaza na kusambaza gesi katika Mikoa mbalimbali kwa kuanza na mikoa ya Dodoma na Morogoro pia kusambaza gesi katika vituo vingine vidogo vitakavyojengwa ikiwemo eneo la Muhimbili na Kibaha na baadaye katika maeneo mengine.

Ameeleza kuwa lengo la mradi huo ni kusogeza karibu huduma ya upatikanaji wa gesi kwa Wananchi ili kuongeza kasi ya matumizi ya nishati hiyo.

Ili kuharakisha ujenzi wa mradi husika amemtaka Meneja wa Usimamizi wa Mradi huo kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania ( TPDC), Mhandisi Aristides Katto kuwepo eneo hilo la mradi muda wote ili aweze kuona na kusimamia kazi hiyo kwa ufanisi na kutoa msukumo kwa Mkandarasi kuharakisha ujenzi huo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mipango na Utekelezaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC ), Derick Moshi amesema kuwa mwezi Septemba mwaka huu kazi za awali za mradi huo zitakuwa zimekamilika, vifaa vitakuwa vimefika nchini na kuanza kusimikwa katika mradi huo.