Makamba: Mradi wa EACOP ni Salama kwa Mazingira


Waziri wa Nishati Mhe. January Makamba amewatoa hofu watanzania juu ya usalama wa Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP) kutoka Hoima Uganda hadi Chongoleani Tanga Tanzania akisema wanaopinga Mradi huo ni wanaharakati wasioitakia mema Tanzania.

Waziri Makamba ameyasema hayo wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa Mradi huo katika Kijiji cha Sojo Wilaya ya Nzega Mkoani Tabora ambapo patajengwa karakana ya kupaka rangi mabomba yatakayotumika kusafirishia mafuta hayo kutoka Uganda hadi Tanga. 

Aidha Makamba amesema wakati wa kutafuta maeneo ya kupitishwa bomba hilo Serikali ilizingatia usalama wa mazingira na usalama wa watanzania huku ikihakikisha bomba hilo halileti madhara zaidi ya kunufaisha watanzania na Taifa kwa ujumla.

Akiongea na Waandishi wa Habari kwenye eneo la Mradi huo katika kijiji cha Sojo Makamba amewataka wakandarasi kutimiza majukumu yao kwa weledi na kutimiza makubaliano waliyoingia na Serikali ili Mradi huo ikamilike kwa wakati uliokusudiwa.

Makamba amesema Mradi huo unaotarajiwa kukamilika mwaka 2025 utazalisha ajira zaidi ya elfu kumi huku ikitarajiwa kuongeza pato la Taifa kutokana na usafirishaji wa mafuta hayo kutoka Uganda na kwenda nchi za nje.