Tpdc Kujenga Bomba La Gesi Jipya Mtwara
Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) limeanza mchakato wa Ujenzi wa
Bomba la gesi kutoka Ntorya hadi Madimba lenye urefu wa kilomita 35.
Mchakato huo umeanza kwa kufanya mkutano wa uhamasishaji kwa wananchi wa
Kata ya Madimba, Moma, Mbawala na Nanguruwe kuhusu ujenzi wa
mradi huo ambao utaanzia Kijiji cha Ntorya.
Akizungumza wakati wa mkutano huo Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Mhe. Dustan Kyobya
amesema hatua ya awali ya utafiti wa mkuza utakaotumika kupitisha bomba
ulishafanyika awali na kubaini vijiji 12 vitakavyopitiwa na bomba.
Vijiji hivyo ni Namayakata, Ngorongoro, Mbawala, Mwindi, Nachenjele, Maili kumi,
Ding’ida, Likweta, Minyembe, Namidondi na Mendachi.
Mhe. Kyobya amesema hatua inayokwenda kufanyika sasa ni zoezi la uthamini wa mali
kwenye mkuza wa bomba wenye upana wa mita 20.
Lengo la zoezi hilo ni kutambua maendelezo yaliyofanyika katika ardhi hiyo ikiwemo
nyumba, mazao na mali zingine ili kubaini thamani yake na kuandaa taratibu za malipo
ya fidia kwa wamiliki watakaopisha mradi huo.
Aidha Kyobya amewataka wananchi wa maeneo ya yanayopitiwa na mkuza wa bomba
kutoa ushirikiano kwa TPDC wakati watakapopita kwenye maeneo yao katika zoezi
uthamini.
”Naomba wananchi muwe wakweli kutoa taarifa sahihi za mmiliki wa eneo na
pia muwape ushirikiano wataalamu watakaopita kwenye maeneo yenu wakati wa zoezi
hilo kuepusha migogoro mbalimbali ya ardhi.’’
Halikadhalika, Mha. Emmanuel Gilbert kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania
(TPDC) amesema utekelezaji wa mradi huo unalenga kuongeza uzalishaji wa nishati ya
gesi asilia kutokana na kuongezeka kwa matumizi ya gesi asilia katika uzalishaji wa
umeme, matumizi ya gesi kwenye magari, matumizi viwandani na majumbani.
- By:Beatrice Peter
- 0 comment