Bodi ya TPDC Yaanza Kazi, Yafanya Ziara Mtwara na Lindi


Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) inayoongozwa 

na Katibu Mkuu Kiongozi Mstaafu, Balozi Ombeni Sefue imefanya ziara ya kikazi 

kutembelea miradi ya utafutaji, uendelezaji na uzalishaji wa gesi asilia katika mikoa ya 

Lindi na Mtwara. 

Akiongea baada ya kuona kazi za ukusanyaji takwimu za mtetemo kwa mfumo wa 3D 

katika kitalu cha Ruvuma kinachoendeshwa na ARA Petroleum Tanzania, Balozi Sefue 

alisema “Matumizi ya gesi asilia hapa nchini yameendelea kukuwa siku baada ya siku 

hivyo kazi inayofanyika katika kitalu hiki inalenga kuongeza uzalishaji wetu wa gesi asilia 

ili kuendana na kasi ya ukuaji wa mahitaji yake”. Balozi Sefue alioneshwa kuridhishwa na 

kazi zinazoendelea katika kitalu cha Ruvuma na kuwaasa ARA Petroleum Tanzania 

kuendelea na kasi hiyo ili kuendana na uwekezaji unaofanyika ndani ya nchi ambao kwa 

kiasi kikubwa unahitaji nishati. 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Dkt. James Mataragio alieleza namna 

TPDC kama mwenye leseni zote za vitalu vya utafutaji wa mafuta na gesi hapa nchini 

anavyoshirikiana na wawekezaji katika mkondo wa juu kuhakikisha shughuli za utafutaji 

na uendelezaji wa rasilimali hizi unaendelea kwa kasi. Dkt. Mataragio alisema “TPDC kwa 

kushirikiana na wawekezaji tumeendelea kufanya kazi mbalimbali za kitaalam zenye lengo 

la kuhakikisha kuwa tunaendeleza sekta yetu ya gesi na mafuta na kuendana na 

ongezeko la mahitaji ya gesi asilia ndani na nje ya nchi”. 

Aidha, Meneja Mkuu wa ARA Petroleum Tanzania, Ndg. Erhan Saygi alieleza mategemeo 

yao kama kampuni ni kuzalisha gesi katika visima vya Ntorya 1, Ntorya 2 pamoja na 

Chikumbi 1 ambacho kiko katika maandalizi ya awali. “Tumepanga kukamilisha kazi ya 

ukusanyaji wa takwimu za mtetemo mwezi Novemba na kuanza kuchimba kisima cha 

Chikumbi 1 ambacho kitakuwa cha tatu katika kitalu hiki mapema mwaka 2023”. Ndg. 

Erhan pia alieleza mategemeo yao ni kuzalisha futi za ujazo milioni 60 kwa simu 

(60mmscfd) kwa kuanzia na uzalishaji utaendelea kukuwa kadri mahitaji ya gesi 

yatakavyokuwa.