India Kuwekeza Kwenye Sekta ya Nishati


Wawekezaji katika sekta ya gesi asilia na mafuta kutoka nchi mbalimbali duniani  wanakutana nchini, kwa lengo la kutafuta fursa za uwekezaji kwenye sekta hizo.

Wakiwa hapa nchini pamoja na mambo mengine, wawekezaji hao wanashiriki kwenye  kongamano la nne la nishati Tanzania linalofanyika Mkoani  Dar es Salaam.

Kando ya kongamano hilo la siku mbili,  Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) Dkt. James Mataragio amefanya majadiliano na wawekezaji katika sekta ya nishati  kutoka nchini India ya  namna ya kuwekeza nchini katika sekta hiyo.

Dkt . Mataragio amesema India imepiga hatua kubwa katika sekta ya gesi na kwamba Tanzania itafaidika  kutokana na ushirikiano baina ya nchi hizo.

“Kwenye kongamano hili tunategemea kupata wawekezaji zaidi ambao watawekeza kwenye sekta ya gesi asilia na mafuta, tayari tumekutana na wawekezaji kutoka India na wameonesha nia ya kuwekeza kwenye sekta ya gesi asilia na gesi ya mitungi,” ameongeza Dkt. Mataragio.