Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), limesaini mkataba wa ushirikiano katika maeneo ya gesi na mafuta na kampuni ya Mafuta ya Taifa (ENH) ya nchini Msumbiji tarehe 09/02/2023 Jijini Dar es salaam.

Mkurugenzi wa Biashara ya mafuta na gesi kutoka TPDC Dkt. Wellington Hudson amesema, kusainiwa kwa mkataba huo ni mafanikio ya ziara ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan nchini Msumbiji na ushirikiano baina ya mataifa hayo mawili.

Mkataba huo wa ushirikiano utahusisha masuala ya ulinzi, kubadilishana utaalamu na mambo mengine ya kimaendeleo.

Kwa upande wake  Mkurugenzi Mtendaji wa ENH, Estevao Rafael Pale amesema, ushirikiano baina ya Tanzania na Msumbiji kupitia sekta ya nishati utasaidia kubadilishana uzoefu kwa manufaa ya pande zote mbili.

Ziara ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan nchini Msumbiji ilifanyika mwezi Septemba, 2022.